NDOA NA FAMILIA

 


Mpendwa msomaji!

Kupitia blog hii tunatamani kuanza kujifunza masuala yanayohusiana na ndoa. Kabla ya kuzama katika mada hiyo nyeti, natamani tuanze kwa kuangalia kanuni muhimu za kufasiri (kutafsiri) maandiko. Kanuni mojawapo inajulikana kama Exgesis. Kanuni hii hutoa hutafsiri kulingana na muktadha wa maandiko husika. Katika kanuni hii, msomaji huanza kwanza kutathmini kama maandiko hayo yamo katika Agano la Kale au katika Agano Jipya. Vile vile kanuni hii inamtaka msomaji kutathmini maandiko kulingana na maandiko mengine yanayozunguka kifungu hicho (muktadha wa karibu) na, kulinganisha na mafundisho yote ya Biblia (muktadha wa kina).

Adeyemo na wenzake (2006 uk 2434) wanatuambia kuwa kadiri kifungu kinachosomwa kinavyokuwa kidogo, ndivyo uwezekano wa makosa ya kutafsiri unavyoongezeka. Maandishi mafupi kwa kawaida huwa na maelezo machache kuhusu mada ya jumla ya kifungu kikubwa. Vile vile, ni muhimu kila tamko lieleweke kulingana na maana yake ya asili katika muktadha wa kifasihi ambamo linatokea kwa sababu muktadha huweka mtiririko wa mawazo, hutoa maana sahihi ya maneno, na pia hufafanua uhusiano sahihi kati ya vitengo, maneno, sentensi na aya.

Kiburi kinapaswa kuepukwa wakati wa kufasiri Biblia kwa kusikiliza wafasiri wengine. Wafasiri wazuri wa Biblia huwa tayari kusikiliza tafsiri za watu wengine. Kama vile chuma hunoa chuma, vivyo hivyo kusikia yale ambayo wengine wanasema juu ya kifungu husika husaidia kunoa fikira za mfasiri. Inatia moyo wengine wanapokubali kile mfasiri anakifikiri. Wanapotofautiana, mfasiri anapewa changamoto ya kuangalia kwa makini kile anachoamini na kisha anaweza kuthibitisha au kurekebisha maoni yake. Kuepuka kiburi ni kanuni muhimu sana katika kufanya ufafanuzi wa dhana zinazojadiliwa kama vile talaka, mke mmoja au mitala.

Nukuu:

Adeyemo, T., Solomon, A., Issiaka C., Tewoldemedhin H., Samuel N., Kwame B., Isabel A. P., Yusufu T., 2006. Africa Bible Commentary. Zondervan.



Comments