NDOA NA FAMILIA
Mpendwa msomaji!
Kupitia blog hii
tunatamani kuanza kujifunza masuala yanayohusiana na ndoa. Kabla ya kuzama
katika mada hiyo nyeti, natamani tuanze kwa kuangalia kanuni muhimu za kufasiri
(kutafsiri) maandiko. Kanuni mojawapo inajulikana kama Exgesis. Kanuni
hii hutoa hutafsiri kulingana na muktadha wa maandiko husika. Katika kanuni
hii, msomaji huanza kwanza kutathmini kama maandiko hayo yamo katika Agano la
Kale au katika Agano Jipya. Vile vile kanuni hii inamtaka msomaji kutathmini
maandiko kulingana na maandiko mengine yanayozunguka kifungu hicho (muktadha wa
karibu) na, kulinganisha na mafundisho yote ya Biblia (muktadha wa kina).
Adeyemo na wenzake (2006
uk 2434) wanatuambia kuwa kadiri kifungu kinachosomwa kinavyokuwa kidogo, ndivyo
uwezekano wa makosa ya kutafsiri unavyoongezeka. Maandishi mafupi kwa kawaida
huwa na maelezo machache kuhusu mada ya jumla ya kifungu kikubwa. Vile vile, ni
muhimu kila tamko lieleweke kulingana na maana yake ya asili katika muktadha wa
kifasihi ambamo linatokea kwa sababu muktadha huweka mtiririko wa mawazo, hutoa
maana sahihi ya maneno, na pia hufafanua uhusiano sahihi kati ya vitengo,
maneno, sentensi na aya.
Kiburi kinapaswa
kuepukwa wakati wa kufasiri Biblia kwa kusikiliza wafasiri wengine. Wafasiri
wazuri wa Biblia huwa tayari kusikiliza tafsiri za watu wengine. Kama vile
chuma hunoa chuma, vivyo hivyo kusikia yale ambayo wengine wanasema juu ya
kifungu husika husaidia kunoa fikira za mfasiri. Inatia moyo wengine
wanapokubali kile mfasiri anakifikiri. Wanapotofautiana, mfasiri anapewa
changamoto ya kuangalia kwa makini kile anachoamini na kisha anaweza
kuthibitisha au kurekebisha maoni yake. Kuepuka kiburi ni kanuni muhimu sana
katika kufanya ufafanuzi wa dhana zinazojadiliwa kama vile talaka, mke mmoja au
mitala.
Nukuu:
Adeyemo, T., Solomon, A.,
Issiaka C., Tewoldemedhin H., Samuel N., Kwame B., Isabel A. P., Yusufu T., 2006.
Africa Bible Commentary. Zondervan.

Comments
Post a Comment